Zambia: Maoni na Hisia Tofauti baada ya Mwakilishi Kutolewa kwenye Mashindano ya Big Brother

Kutolewa kwa mwakilishi wa Zambia, mwanamuziki maarufu anayefahamika kama Mampi, kutoka kwenye mashindano yanayoendelea hivi sasa ya Big Brother Africa toleo la saba, kumepokelewa kwa hisia na maoni tofauti na raia wa mtandaoni.

Big Brother Africa: StarGame ni toleo la saba la mfululizo wa vipindi vinavyorushwa moja kwa moja kuhusu maisha ndani ya jumba la Big Brother, ambapo yatarushwa kwa muda wa siku 91 na mshindi atajinyakuliwa dola 300,000 (sawa na Tsh500 milioni). Mfululizo wa mashindano hayo unatarishwa na Endemol nchini Afrika ya Kusini, ambapo maonyesho haya ya moja kwa moja ya mashindano hayo kwa njia ya televisheni yametokea kuwa maarufu zaidi barani Afrika.

Jina halisi la Mampi ni Mirriam Mukape. Baada ya kuwa kwenye nyumba hiyo ya Big Brother kwa majuma matatu, washindani wenzake walipendekeza atolewe. Wakati ambapo watu wengi wana maoni kwamba mwanamuziki huyo — ambaye anafahamika zaidi kwa muziki wake wenye miondoko ya kingono awapo jukwaani — alikuwa akiangusha heshima ya taifa lake kwa jinsi alivyokuwa akiendesha maisha yake kwenye maonyesho hayo ya moja kwa moja kwenye televisheni, wapo waliojenga hoja kwamba uzoefu wake kwenye nyumba hiyo ulisaidia kumkomaza “kwa kumpa mtaji wa kiuhusiano.”

Mara tu Zambian Watchdog ilipotangaza habari za hivi punde Kuondoshwa kwa Mampi, wasomaji wengi hawakusita kumlaani mwanamuziki huyo.

Mampi

Picha ya Mampi kutoka kwenye moja ya picha za televisheni akiwa ndani ya nyumba ya BBA. Picha kwa hisani ya ukurasa wa Facebook wa Paramaunt Spit&#39

Msomaji mmoja, Gloria, wala hakumung'unya maneno pale alipomlinganisha na mshiriki mwingine kutoka Zambia aliyeshinda moja ya zawadi za ufunguzi wa BBA, Cherise Makubale:

Ama kwa hakika ametia aibu sana, kinyume kabisa na Cherese, hebu msikilize kwenye picha hii ya video kwenye youtube: http://www.youtube.com/watch?v=P2w0EjH15q8

Msomaji mwingine, Violet aliandika:

Yippee nafurahi sana kwamba ametolewa, maana alikuwa na roho ya kwa nini na mmbeya. Sijui hata kama anajijua alivyo…..Hiloooo Mampi wala hatutakukumbuka uuuo….Sasa Maneta hana budi kufuata baada yake maana amekuwa kama nyuki mdogo anayeghasighasi BZZZZZZZ…. na huo siyo mwisho…. Tabia njea na utu hawana sifa hizi …..Kwa heriiii

Said Ras-Kadafi alikuwa na haya ya kusema kuhusu kuondolewa kwa Mampi:

Kwa kusema kweli, inashangaza mno? Nyie ndiyo hamwelewi, kama tulivyo tulio wengi, Mampi ni binti wa kutoka wamukomboni [makazi yenye msongamano mkubwa wa watu na yaliyo maskini — Uswazi], hamwezi kuniambia kwamba mlitumaini Mampi afaye vizuri, tena nafikiri wiki 2-3 ni muda mrefu sana kwa Mampi, yeye amezoea kuonyesha maungo yake ya siri hadharani na papo hapo mnajenga matumaini kwake, ninachosema ni kuwa kuna watu wanaojua kuonyesha tofauti kati ya maisha ya kuigiza na maisha ya kweli, lakini si Mampi, yeye sanasana ni nusu mwanamuziki na nusu mkaa uchi hadharani, Mungu ashukuriwe kwa sababu hatukuona makubwa kabla hajatolewa na kurudi nyumbani.” […]

Msomaji mmoja, Ndumeleti, aliamua kumtetea akisema:

Hivi, hawa jamaa wanatazama vipindi gani? Kwa kusema ukweli, Mampi katika nyumba ile ya Big Brother alikuwa na mwenendo bora kuliko baadhi ya wenzake aliokuwa nao mle, mathalani, Zainab, Lady May na hata Maneta. Ukizungumzia kucheza muziki, sawa, lakini suala la kubaki utupu … jambo hili linanikumbusha sakata la Chansa Kabwela! Watu wa Zambia, hebu jifunzeni kuwaunga mkono walio wenu. Ameondolewa kwenye mashindano kwa sababu nini Wazambia mlipachika alama kama malaya na mtu mbaya na hamkumpigia kura. Katika nyumba ile alijitahidi sana kuwa mstaarabu kadiri alivyoweza hasa ukizingatia mazingira yenyewe, hebu fikiri hata hakujaribu kunywa pombe. Hivi hamjamwona Zainab akivua nguo zake zote au akicheza muziki huku amevaa chupi tu tena mbele ya kamera! Amkeni jamani! blockquote>

Lakini ni mwanamuziki mwenzake, Saboi Imboela, anayesoma shahada ya uzamili nchini New Zealand, aliyetetea mwonekano wa Mampi katika BBA kupitia ukurasa wake wa Facebook:

Hongera Mampi (mwanetu) kwa kukuza ‘mtaji wako wa kimahusiano’. Baada ya kuwa kwenye maonyesho ya BB, unakuwa kama vile umepitia kwenye chuo kikuu katika ulimwengu wa kitaaluma. Hapo kabla, ni watu milioni 13 tu wa Zambia waliokufahamu lakini sasa hivi Afrika nzima inakufahamu. Siyo hasa shahda au mtaji wa kimahusiano alionao mtu unaomfanya kuwa mkubwa, ni nini anachofanya nao au anavyopanga kuutumia ndiyo inayomtofautisha mtoto na mtu mzima. Maisha yako yamebadilika daima mara tu ulipojiweka wazi mbele ya Afrika katika wiki hizo chache, kwa hiyo jinsi utakavyoutumia mtaji huo, hiyo ni juu yako. Mwisho, mimi binafsi nitafanya kila ninaloweza kumshawishi mume wangu na wadhamini wetu ili wewe ushike nafasi ya mhusika mkuu katika mradi tunaoupanga. Tunaingia gharama kubwa sana kuwatumia waigizaji kutoka Nigeria kwa sababu hatukuwa na Mzambia mwenye sifa za kinyota aliyefahamika katika bara zima. Sasa kwa vile tumekupata wewe na tunaweza kuuza kazi hiyo hata katika nchi nyingine kwa sababau wewe utakuwemo ndani yake na kwa sababu ‘mtaji wako wa kimauhusiano’ umekua … Kwa hiyo, kuna watu ambao huwa wanafurahia kuona kwamba mtu hakufika mbali sana katika mashindano makubwa kama ya Big Brother, lakini wanafanya hivyo kwa sababu ya ufinyu wao wa kufikiri na hawajui ni kwa jinsi gani mtu anaweza kunufuika mara nyingi mno na kupitia jambo kama hilo – kwa hiyo nani ni fisi? … Ninajivunia sana kwa ajili yako wewe ni mwana wetu …umetengenezwa kwa chuma cha pua.

Mwanamtandao mwingine, Isaac Mwanza, vilevile kupitia ukurasa wake wa Facebook, aliongeza mtazamo wa kisiasa Wanawake wa Zambia washindwa kumwunga mkono mwanamke mwenzao:

Mampi Mukape alikataliwa na watu wake mwenyewe na wanawake wa Zambia walikuwa mstari wa mbele katika kumpiga vita. Nafikiri ni jambo la kufikirika hivi sasa kuwaunga mkono wanawake wa Zambia hasa kwa sababu hawawezi kuungana mkono wao kwa wao. Hebu sote basi tumwunge mkono Roki wa Zim (Zimbabwe) au Prezzo wa Kenya katika kinyang'anyiro cha BBA!

Katika mtandao mwingine wa habari za kiraia, Tumfweko, mchungaji mfawidhi aliandika:

Tafadhali Wazambia wenzangu, hebu tujaribu kumwunga mkono yeyote yule anayeiwakilisha nchi yetu nzuri ya Zed. Mimi nilisikitika sana kuona kwamba ni asilimia 1 TU ya kura ndiyo ilitumwa na raia wa Zed, lakini hebu tazameni Afrika ya Kusini, yaani licha ya madudu anayofanya mwakilishi wao kwenye nyumba ile bado wanampigia kura kibao kila siku, wanamwunga mkono wa asilimia 100. Hiyo inaonyesha jinsi gani wale jamaa wameungana. Hali iko hivyo hivyo kwa Wanaigeria, Waghana, Wabotswana, yaani kwa kutaja wachache tu. Kwa hiyo, tafadhali, raia wenzangu wa Zedi hebu tuige wanavyofanya watu wa nchi nyingine na kuwaunga mkono wawakilishi wetu wengine waliobaki katika mashindano ya BBA. Ninafahamu jinsi wawakilishi kutoka Zedi wanavyoogopwa mle kwa sababu ya uwezo wao mkubwa. Mungu aibariki Zed!!

Vile vile kupitia Twita, wanamtandao wamekuwa na maoni tofauti:

@ChibuyeK: RT @skrypted: Wapendwa wachochezi, kwa kweli Mampi amefanya kitu na ameonekana kwa watu wengi wakati ambapo ninyi mlipoteza saa kibao kumwangalia & lt; na amejipatia pesa pia

Nyingine ilisema, huku ikiwa na matumaini kwa Mzambia mwingine anayeshiriki kwenye BBA, akisema:

@DJLBCZambia: Sasa kwa vile huyo Mampi ametoswa, hata hamu yangu ya kufuatilia BBA imedorora, lakini hebu ngoja kwanza, bado tunaye binti ya Paul Ngozi [Mwanamuziki wa Zambia aliyefariki miaka 20 iliyopita] katika mashindano.

Anza mazungumzo

Mwandishi, tafadhali jiandikishe »

Miongozo

  • Tafadhali wape heshima watumiaji wengine. Maoni yenye lugha ya chuki, matusi na mashambulizi binafsi hayataruhusiwa.