Moroko: Kupinga Mateso Sehemu Moja; Kupinga Mateso Kila Sehemu

Katika juma hili, maofisa wa Moroko wamekuja juu sana huku wakimiminika kwenda mbele ya kamera ili kueleza kukasirishwa kwao kutokana na kukamatwa na pia kile kinachohisiwa kuteswa kwa Mustapha Salma Ould Sidi Mouloud [Fr] kulikofanywa na Kundi la Polisario, ambalo ni vuguvugu linalotaka kujitenga na Moroko na linaungwa mkono na nchi ya Aljeria ili kutawala sehemu ya Sahara Magharibi. Mustapha Salma, ambaye hapo kabla alikuwa chifu wa jeshi la polisi na kiongozi wa ngazi ya juu katika Kundi la Polisario alituhumiwa kwa uhaini na kundi hilo linalotaka kujitenga hasa baada ya yeye kusifu hadharani mpango wa kuwa na uhuru zaidi wa kujiamulia [Ar], ] unaopendekezwa na raia wengi wa Moroko ili kutatua mgogoro huo uliodumu kwa zaidi ya miongo mitatu. Ni vigumu kutokuitilia maanani habari hii ya Mustapha Salma hasa kwa kuwa imechapishwa sana na vyombo vya habari vya Moroko; huku picha zake zikipamba kurasa za mbele za magazeti ya hapa. Vyombo vya habari vya dola vimelaani vikali Kundi la Polisario na waungaji wao mkono wa nchini Aljeria kwa madai kwamba Kundi hilo limekiuka haki ya Mustapha Salma ya kujieleza huku vikieleza kuhofia kwamba huenda anateswa. (Mustapha Salma hata hivyo, anaripotiwa kwamba tayari ameachiwa huru.)

Wakati ambapo habari hii inaibua masuala muhimu na ya msingi kuhusu ukiukwaji wa haki za binadamu unaofanywa na Kundi la Polisario na utawala wa Aljeria, baadhi ya wanablogu walionyesha hasira yao dhidi ya upuuzaji ambao ulifanywa na vyombo vikuu vya habari na Serikali ya Moroko kuhusu majaliwa ya raia kijana wa Moroko, Fodeil Aberkane. Ni habari ya nchini humuhumu lakini ni ya kutisha inayomhusu kijana huyu mdogo, ambaye hata haki zake za msingi kabisa za kibinadamu, ikiwemo ile haki ya kuishi, amenyang'anywa.

Mhanga huyu alikuwa na umri wa miaka 37 na kifo chake baada ya kuteswa vibaya katika kituo cha polisi katika mji wa kale wa Salé ulio karibu na jiji la Rabat, ni jambo ambalo wanablogu wengi wanalichukulia kuwa mabaki ya enzi za Miaka ya Chuma, ambazo zilikuwa kipindi kibaya cha utawala wa Mfalme Hassan II, ambapo ukatili wa polisi na utesaji uliopangwa na kufanywa na vyombo vya dola ulikuwa wa viwango vya kutisha na ambao raia wa Moroko walilazimika kuuishi.

Fodeil alikamatwa mnamo tarehe 11 Septemba 2010 akituhumiwa kutumia bangi. Baada ya kukaa jela kwa saa 48, jaji aliamuru kwamba aachiwe huru. Siku chache baadaye Fodeil alikwenda kituo cha polisi ili kuomba arejeshewe mali zake: pikipiki na simu ya mkononi. Kulitokea majibizano pale kituoni na Fodeil alijikuta akitupwa tena gerezaji, akituhumiwa “kuwatukana maofisa wa polisi wakati walipokuwa wakitimiza wajibu wao.” Siku mbili baadaye alihamishiwa hospitali kuu jijini Rabat ambapo baadaye alitangazwa kwamba amefariki dunia. Hakuna mashaka katika akili za familia ya Fodeil na marafiki zake kwamba nini hasa kilimpata kijana huyo mpaka kukutwa na mwisho huo mbaya [Fr]: ni ukatili wa polisi na mateso wanayowafanyia watu. Upelelezi tayari umetangazwa kuanza hata hivyo hakuna mashitaka yaliyofunguliwa dhidi ya yeyote yule anayeaminika kuhusika na kifo cha Fodeil Aberkane.

Habari hiyo imenasa macho ya wanablogu na wanaharakati wengine wa mtandaoni hasa katika kipindi hiki ambapo uhuru wa vyombo vya habari uko katika hali tete nchini humu na wakati huo huomwandishi na mwanablogu Laila Lalami anatukumbusha, kwamba hilo siyo tukio pekee:

Kilichompata Fodeil Aberkane si yeye tu. Katika miaka michache iliyopita, shutuma za utesaji zimetolewa dhidi ya polisi nchini Moroko mara nyingi tu. Miaka miwili iliyopita, Zahra Boudkour, mwanafunzi wa chuo kikuu huko Marrakech, mwenye umri wa miaka 21, alikamatwa kwa kushiriki kwake kwenye maandamano ya wanafunzi. Alivuliwa nguo na kupigwa , lakini mpaka sasa hakuna yeyote aliyeletwa mbele ya sheria kwa ukatili huo aliofanyiwa binti huyo. Katika makutano na polisi wa Marrakech, mwanafunzi mwingine wa chuo kikuu, Abdelkebir El Bahi, alijikuta akitupwa kutoka orofa ya tatu kupitia dirisha la bweni. Hivi sasa habanduki kutoka kwenye kiti cha matairi cha walemavu, na hili litakuwa jambo la maisha yake yote. Boudkour na El Bahi waliteswa na kuhujumiwa kwa sababu tu ya kuamini na kuwa na fikra tofauti. Fodeil alichofanya ni kujaribu tu kupata tena pikipiki yake.

Bill Day akiandika kwenye the a la menthe anakubaliana:

Kwa sababu wahanga (wa aina hii) si watu mashuhuri, basi wanateseka na kufa pasipo habari kuvifikia vyombo vya habari vya Magharibi – ni kama wanavyosema, kama haupo machoni basi huna nafasi akilini. Wakati ambapo ufalme katika enzi za “Miaka ya Chuma” ulikiuka haki nyingi za binadamu tena hadharani, na katika kipindi ambapo kulikuwa na utesaji mkubwa wa wapinzani wa kisiasa chini ya Mfalme Hassan II, matukio kama yale yaliyoripotiwa na Lalami ni vipengele visivyopendeza kwa utawala uliopo sasa unaojitia kuwa na sura angavu na mafanikio, hasa kwa kuzingatia kwamba unatokea sanjari na ukandamizaji wa uhuru wa vyombo vya habari.

Mwanablogu na mwanaharakati Najib Chaouki [Ar] aliandaa ukurasa wa Kundi la Facebook aliouita “Sisi sote ni Wahanga wa Mateso,”ambapo katika utangulizi alitoa mwito kwa “watekelezaji wote wa makosa ya utesaji wafikishwe mbele ya sheria na kuhukumiwa kiadilifu.”

Mwanablogu Larbi analaani unafiki wa serikali ya Moroko [Fr]. Anaandika:

Si ce gouvernement, avait une seule once de dignité, il devrait différer le plus tôt possible les assassins de Fodail Aberkane devant la justice ne serait-ce que pour ne pas mourir du ridicule. Quant à la torture, on oserait même pas penser qu’elle cessera un jour, tant qu’au Maroc , elle est apparemment éternelle.

Kama serikali hii ingalikuwa na chembe ya utu hata kidogo, basi ingaliwafikisha wauaji wa Fodeil Aberkane mbele ya haki haraka iwezekanavyo, ili kuepuka kuchekwa mpaka kufa. Kwa upande wa mateso, hatudhani kwamba hali hiyo itakoma, maana inaonekana kama ni hali ya kudumu nchini Moroko.

Harakati za mtandaoni za kutoa mwito wa “Kukomeshwa kwa Utesaji Unaofanywa na Polisi nchini Moroko,” tayari umekwishapata uungwaji mkono kwa sahihi zipatazo 300 mpaka sasa.

Baadhi ya wanablogu na watumiaji wa Twita wamekuwa wakirushiana matangazo na picha mbalimbali kama picha hii yenye maandishi: “Makhzen: Police kills. If you wish it to continue, keep quiet.”



(yaani “Makhezan: Polisi Waua. Kama unataka kubaki hai, basi funga mdomo.”)

Makhzen ni istalahi inayotumika kuelezea utawala uliojisimika wa Moroko.

Mwanablogu na mwanasheria Ibn Kafka anapendekeza watu wasome alichokiandika [Fr] kuhusu kwa nini matukio ya utesaji nchini Moroko yamekuwa hayakomi:

La torture est […] un instrument de pouvoir dont le régime marocain ne tient pas à se passer, mais dont il tient seulement à limiter les effets nocifs sur sa réputation, nationale et internationale. En l’absence de contre-pouvoirs politiques et institutionnels sérieux en interne, ce sont principalement les retombées médiatiques et diplomatiques externes qui pèsent sur les choix sécuritaires du makhzen.

Mateso ni nyenzo ya mamlaka ambayo utawala wa Moroko hauko tayari kuiachia, lakini papo hapo inataka kudhibiti madhara ya nyenzo hiyo katika kutunza sifa yake ndani na nje ya nchi. Kwa kuwa hakuna upande wa ndani wa kisiasa au kitaasisi wenye kuleta mizania ulio makini, basi ni kutofautiana kunakoletwa na vyombo vya habari na ule wa kidiplomasia ambao ndiyo unakwaza maamuzi yanayohusiana na usalama wa Makhzen.

Kuhusiana na vyombo vya habari vya Magharibi, mwanablogu huyu anasema …

[Ils] ne s’intéressent au Maroc qu’à travers l’optique orientalisme-islamisme-terrorisme – et dans cette optique, Fodail Aberkane ne remplit pas de fonction utile.

Vinaitazama Moroko kwa kupitia lensi za umashariki – na kwa sababu hii, Fodail Aberkane hakidhi manufaa yoyote kwao.

Madaraka na uwezo mkubwa kupita kiasi usiokaguliwa walio nao polisi unawafanya watumie vibaya madaraka yao, kama anavyoandika Riad Essebai kupitia Blog ya Robin des [Fr]:

Aberkane n'est ni le premier, ni le dernier à être la victime d'un système, ou l'agent de la force publique peut être, à la foi, juge et arbitre. Ce pouvoir “absolu”, est le véritable criminel dans cette affaire, et c'est cela qu'il faudra combattre.

Aberkane si mhanga wa kwanza wala wa mwisho wa mfumo ambamo askari polisi ndiye hakimu na mpatanishi. Mamlaka haya “yasiyo na ukomo” ndiyo hasa mkosaji wa kweli katika kisa kama hiki, na hiki ndicho ambacho hatuna budi kukipiga vita.

aboulahab, akiandika kupitia blogu ya C.J.D.M. [Fr] (Circle of Young Moroccan Idiots, yaani Mduara wa Wapumbavu Vijana wa KiMoroko) anawahimiza watu kuvunja ukimya:

[L]’Histoire retiendra tout type de profil, sauf le profil bas. Assez de bassesse. Le Maroc a besoin de grands hommes, qu’ils se manifestent. Sommes-nous déjà une civilisation de fonctionnaires asservis et de citoyens muets ?

Historia itawakumbuka watu wote isipokuwa watu wasiotaka kujitokeza na kuzungumza. Unatosha uzubaifu huu. Moroko inahitaji watu wenye mioyo ya kishujaa. Hebu na wajitokeze watu hao. Je, sisi ni ustaarabu wa watumishi wa serikali na raia walio mabubu na waliokandamizwa?

Anza mazungumzo

Mwandishi, tafadhali jiandikishe »

Miongozo

  • Tafadhali wape heshima watumiaji wengine. Maoni yenye lugha ya chuki, matusi na mashambulizi binafsi hayataruhusiwa.