Bolivia: Uhaba wa Maji Kwa Sababu ya Theluji Inayoyeyuka

Safu ya milima ya Chacaltaya ina baadhi ya vilele ambavyo ni alama zenye maana katika safu ya milima Andes iliyopo Bolivia. Kwa kuwa ilikuwa ni sehemu moja pekee ambapo mchezo wa kuteleza barafuni uliweza kufanyika katika nchi hii ya milimamilima, milima hii ni maarufu sana kwa wale walio kwenye Idara ya La Paz, na pia kwa wageni wapenda kuvumbua mambo mapya. Ni katika milima hiyohiyo ambapo zilifanyika mechi za soka za hisani ambazo kwazo Rais Evo Morales alishiriki ili kuthibitisha kwamba michezo inaweza kuchezwa katika maeneo ya ukanda wa juu.

Hata hivyo, theluji ya Chacaltaya imeanza kupungua kwa kasi inayotisha na kali sana. Athari ya mabadiliko ya hali ya hewa kwa barafu iliyoko kwenye mlima huu na mingine iliyo katika eneo hili zimekuwa zikichunguzwa na Profesa wa Chuo Kikuu cha San Andrés, Edson Ramírez, ambaye anahitimisha kwa kusema kwamba kuna uhusiano wa moja kwa moja kati ya kuongezeka kwa kiwango cha joto na kutokweka kwa theluji au barafu hiyo.

Ramírez na timu yake wamekuwa pia wakitafiti barafu iliyoko kwenye mlima mwingine ambao nao umekuwa ukipatwa na athari zinazofanana na huo mwingine na madhara ya mwenendo huo kwa jamii inayoishi maeneo ya jirani. barafu iliyoko kwenye mlima unaoitwa Tuni Condoriri glacier unayeyuka katika kasi kubwa, hivyo kuwaathiri wapenzi wa alpine, lakini pia hali hiyo inaathiri jamii za wahamiaji walio katika hatari ambao huitegemea ili kujipatia maji ya kunywa na kwa ajili ya shughuli za kilimo.

Tenki la kuhifadhia maji yanayotoka kwenye barafu iliyoko kwenye mlima huo hutoa kiasi cha 80% cha maji ya kunywa kwa jiji la El Alto na vitongoji vyake vya La Paz. Kwa mujibu wa sensa ya hivi karibuni, El Alto ina jumla ya watu wapatao 827,000 [es],ambapo idadi hiyo inakua kwa 5.1% kila mwaka. Kwa mujibu wa mwandishi wa habari na mwanablogu Mónica Oblitas, kiwango hiki ni zaidi ya mara mbili ya wastani wa taifa [es]. Wataalamu wanabashiri uhaba wa maji na kulipia maji, ambapo watu wengine wanabashiri kwamba suala la mgao wa maji limekaribia [es]. Timu kutoka Observador Global [es] (Wafuatiliaji wa Ulimwengu) waliandaa makala ya video yenye sehemu sita kuonyesha madhara ya upungufu wa maji katika eneo hilo.

Jiji hilo ni makazi ya wahamiaji kutoka jamii za wenyeji wa Aymara katika Altiplano ya Bolivia, ambao huhamia katika jiji la El Alto, mara nyingi wakiwa katika hali ya umaskini uliokithiri. Mwanablogu wa Ki-Bolivia, Cristina Quisbert anayeandika katika blogu ya Indigenous Bolivia anaelezea hali inayowakabili wakaazi wengi hususani kuhusu maji salama ya kunywa:

Kuna mambo mengine yanayochangia katika ugumu wa kupata maji. Watu wengi wanafika kutoka vijijini kuingia katika jiji la El Alto na kuanzisha makazi pale wanapoweza kufanya hivyo. Kwa sababu ya ukosefu wa fedha, wanaishi popote pale mara nyingi ambapo hapana maji ya kunywa wala hakuna mfumo wa maji taka. Baadhi yao huchimba visima vifupi vya hadi mita tatu hivi hadi wapate maji. Kwenye mwezi Novemba hivi, mvua za mwanzo huanza kunyesha, hivyo kufanya uwezekano wa kupata maji kwa majirani hawa. Mwishowe, uhaba wa maji huchangia katika kuongeza umaskini na vyote hivyo husababisha maradhi.

Kuna hali fulani ya mambo mbalimbali na tofauti kuwa pamoja . Mimi napata maji nyumbani lakini jirani zangu hawapati. Hili ni jambo zito kwa familia. Kwa upande wangu, ninawagawia maji familia nyingine. Basilio naJuana wana watoto wanne. Wanaishi katika nyumba ya kupanga. Nyumba wanamoishi haina maji yanayofaa kunywa. Kila wanapoyahitaji, basi hawana budi kutumia mpira ili kupata maji kutoka nyumbani kwangu na mwisho wa mwezi basi tunagawana gharama kadiri ya ankra.

Hata hivyo, siyo tu kwamba Tuni Condoriri hutoa maji ya kunywa kwa ajili ya jiji hilo tu, lakini pia hutoa maji kwa ajili ya shughuli za kilimo kwenye safu za Altiplano. Endapo uendelezaji wa shughuli za kilimo utapungua kwa sababu ya uhaba wa maji, watu wengi zaidi kutoka maeneo ya vijijini watatiririka kwenda El Alto kujitafutia maisha, ambapo watakumbana na tatizo lile lile la uhaba wa maji na papo hapo wakiongeza mahitaji ya maji.

Wanaharakati wa 350.org wakikwea kwenye mlima barafu Chacaltaya huko Bolivia kufanya maandalizi ya tukio kubwa mnamo tarehe 24 Oktoba. Picha imetumika chini ya leseni ya haki miliki huru.

Wanaharakati wa 350.org wakikwea kwenye 'mlima' barafu Chacaltaya huko Bolivia kufanya maandalizi ya tukio kubwa mnamo tarehe 24 Oktoba. Picha imetumika chini ya leseni ya haki miliki huru.

Ni sura inayopewa kipa umbele ya barafu iliyoko kwenye mlima wa Chacaltaya ndiyo inayovuta usikivu wa ofisa wa serikali za mitaa na vikundi vingine vya wanaharakati ili kutazama tatizo la mabadiliko ya hali ya hewa katika ukanda wa Bolivia. Tukio lililotokea mahali hapo siku za hivi karibuni lililohusiana na kampeni ya 350.org lilitangazwa katika Facebook [es], likiwaalika raia wa Bolivia kutembelea ‘mlima’ barafu wa Chacaltaya kujionea wenyewe madhara yanayofanyika.

Hatimaye, Oblitas anahitimisha kwa swali hili lifuatalo [es]:

Chacaltaya ya no está y pronto dejarán de existir otros glaciares, ¿está el país preparado para esas pérdidas?, ¿somos conscientes de la importancia de tomar un rol activo e inmediato contra el calentamiento? Para muchos, el cambio climático no es un fenómeno global y no creen sentirse afectados, pero lo cierto es que absolutamente todos estamos en riesgo y no todos podemos enfrentarlo en las mismas condiciones. La lucha continúa, aunque ya sea tarde para lugares como Chacaltaya.

‘Mlima’ barafu wa Chacaltaya haupo tena, vilevile hivi karibuni ‘milima’ barafu mingine nayo itatoweka. Je, nchi iko tayari kupata hasara hii? Je, tunatambua umuhimu wa kuchukua wajibu wa haraka wa kushiriki kukabili kuongezeka kwa joto duniani? Kwa walio wengi, mabadiliko ya hali ya hewa si tatizo la kiulimwengu na hawajihisi kuathiriwa, kila mmoja yuko kwenye hatari ingawa si kila mmoja anaweza kukabiliana na hatari hiyo kwa namna moja. Mapambano yanaendelea, hata kama tayari tumechelewa katika maeneo kama Chacaltaya.

Anza mazungumzo

Mwandishi, tafadhali jiandikishe »

Miongozo

  • Tafadhali wape heshima watumiaji wengine. Maoni yenye lugha ya chuki, matusi na mashambulizi binafsi hayataruhusiwa.